Hii  Ndiyo Siri ya Kuwa Mhubiri Bora

Rafiki yangu mpendwa katika Kristo,

Mojawapo ya wajibu mkuu ambao Mungu amelikabidhi kanisa ni kuhubiri Injili, yaani kueneza habari njema za wokovu. Ni agizo alilolitoa Yesu kwa wafuasi wake. “Akawaambia, Enendeni ulimwenguni mwote, mkaihubiri Injili kwa kila kiumbe “(Marko 16:15).

Kutokana na idadi ndogo ya wachungaji katika makanisa mengi, mahubiri mengi makanisani na yale ya hadhara hufanywa na walei. Walei ni waumini wanaofanya kazi ya Bwana, kama vile kuhubiri injili, lakini hawajapata elimu yoyote ya kazi hiyo na mara nyingi huwa wanafanya kazi hiyo kwa kujitolea bila malipo au kwa malipo kidogo. Pamoja na ukweli kwamba mahubiri mengi hufanywa na walei, lakini si kila muumini mlei anaweza kuhubiri na waumini wengi hupata taabu sana kila wanapotakiwa kuhubiri.

Hata wale wenye kipaji cha kuongea na kuvuta watu, wanapotakiwa kuhubiri huwa wanapata taabu pia. Hii ni kwa sababu si kila mtu anayeweza kuongea anaweza kuhubiri.  Unaweza kujiuliza, nini kinasababisha hali hii? Kinachosababisha hali hii ni kwamba kuhubiri ni sanaa na sayansi yenye kanuni na mbinu za kuzingatia. Usipojua kanuni na mbinu hizo unaweza ukahubiri lakini usifikishe ujumbe vizuri kama ulivyokusudia. Yaani, ujumbe ukatoka kwako lakini usifike kwa hadhira vizuri. 

Ninaposema kuwa unaweza ukahubiri lakini usifikishe ujumbe kwa hadhira, ninamaanisha kuwa ujumbe wako unaweza usieleweke vizuri. Unaweza pia usifikishe ujumbe kwa hadhira ikiwa hautaweza kuvuta usikivu wa watu. Kama hutaweza kuvuta usikivu wa watu, ujumbe wako nao hautawavuta na hivyo wanaweza wasiusikilize na wasipate kile ulichokusudia wapate.

Kwa sababu kuhubiri ni Sanaa na sayansi, ndiyo maana wahubiri wanatofautiana. Wapo wanaoweza kueleweka vizuri na wapo wasioweza kueleweka vizuri licha ya kwamba wahubiri wote hutumia biblia kuwasilisha ujumbe wao. Zaidi ya kutumia biblia, wahubiri wote huomba sala wakati wa kuandaa mahubiri yao na hata wakati wanapotaka kuanza kuhubiri. Wanafanya hivyo ili kupata nguvu na uwezo wa Mungu ili wafikishe ujumbe wao vizuri.

Kwa sababu kuhubiri ni Sanaa na Sayansi, ndiyo maana baadhi ya wahubiri wanaweza kuhubiri hata masaa mawili na usichoke kuwasikiliza na mahubiri yao unaweza kuendelea kuyakumbuka kwa miaka kadhaa. Ni dhahiri, mahubiri ya aina hii yanaweza kumgusa mtu na kumsaidia kukua kiroho. Lakini kuna baadhi ya wahubiri wanapohubiri, dakika tano tu zinatosha kuwafanya waumini waanze kusinzia na mahubiri yao yanaweza kusahaulika hata ndani ya siku moja tu. Mahubiri ya aina hii yanaweza yasiwe na mguso katika ukuaji wa kiroho.

Kwa sababu Kuhubiri ni Sanaa na Sayansi, kuna haja kubwa ya kujifunza sanaa na sayansi hiyo.  Sayansi na Sanaa ya kuhubiri inaitwa Homilia. Kwa kifupi, Homilia ni maarifa juu ya namna ya kuandaa na kuwasilisha mahubiri kwa hadhira. Kwa kujifunza Homilia, wale wanaopata taabu wanapotakiwa kuhubiri, wanaweza kupata mbinu na kanuni za kuandaa na kuwasilisha mahubiri na kuwa wahubiri wazuri.

Hata wewe, unaweza kujifunza Homilia

Kwa kuwa kuhubiri ni wajibu wa kila muumini, basi kila muumini anapaswa kujifunza Homilia. Kama unataka kujifunza Homilia, unaweza kujipatia kitabu kizuri kiitwacho Homilia kwa Walei: Ustadi wa Kuandaa na Kuwasilisha Mahubiri. Kitabu hiki kinamfaa kila muumini mlei. Hata walei ambao wana kipaji cha kuhubiri na wamekuwa wakihubiri, bado wanahitaji kujifunza zaidi ili kuboresha uwezo wao. Hivyo, kitabu hiki kitawafaa wao pia.

Kitabu hiki kimeandikwa kwa namna ambayo ni rahisi kueleweka kwa walei na kina mambo muhimu tu ya kufanyia kazi na hakijaingia kwa undani katika nadharia nyingi za kihomilia zisizohitajika ili waweze kujisomea wao wenyewe na kuelewa.

 Kitabu hiki kinawafaa watu wote wanaohubiri Neno la Mungu katika maeneo mbalimbali kama vile katika ibada ya kawaida kanisani, ibada maalum za kanisani kama vile ibada ya maombi katikati ya juma, mikutano ya uamsho na majuma ya maombi, mahubiri ya hadhara na matukio mengine ambapo mahubiri hutolewa.

Ili kupata kitabu hiki, wasiliana nasi kupitia namba za simu; +255754-405582 (Simeon Shimbe), au  +255714-606278 (Devotha Shimbe) na kwa E-mail kwa anauwani zifuatazo: spshimbe@gmail.com na devothashimbe@gmail.com.

Je, unataka kupata mafunzo endelevu kuhusu mafaniko kwa mkristo?

Kama unataka kuendelea kujifunza kuhusu masuala mbalimbali juu ya mafanikio kwa mkristo unaweza kujiunga na mtandao huu ili uweze kupata makala mbalimbali. Kwa kufanya hivyo, utapata makala kupitia email yako kila zinapowekwa katika mtandao huu.

Ili kujiunga, jaza fomu niliyoko hapa chini.

About Simeon Shimbe

Simeon Shimbe ni mchumi kitaaluma, mwandishi wa vitabu na makala na mjasiriamali. Amekuwa akiandika kuhusu masuala ya fedha, biashara na uwekezaji na masuala mbalimbali ya kiroho.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *