Kwa Nini Watu Wengi Wanapenda Kuajiriwa Licha ya Ajira Kutowapatia Mafanikio ya Kifedha?

Rafiki yangu mpendwa katika Kristo,

Wafanyakazi wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania bado wanasikilizia maumivu baada ya kupata pigo kubwa mwezi huu. Pigo hilo ni nyongeza ndogo ya mshahara isiyolingana na matarajio yao na isiyolingana na hali halisi ya ugumu wa maisha uliopo.

Wafanyakazi wa Serikali walitangaziwa na Rais wa Jamahuri ya Muungano wa Tanzania kwamba wangeongezewa mshahara kwa asilimia 23 lakini walioongezewa kwa asilimia hiyo ni wafanyakazi wa kima cha chini tu na wengine wameongezewa kwa asilimia ndogo sana. Hali hii imewafanya walalamike sana na kuibua mjadala mkali kwenye mitandao ya kijamii na kwenye ofisi za Serikali.

Kutoka na mtafaruku uliotokea, serikali imelazimika kukutana na viongozi wa shirikikisho la vyama vya wafanyakazi ili kufafanua ongezeko la mshahara lilifanyika nap engine kuwatuliza ili wasiendelee kuibua mtafaruku. Kwa taarifa zilizotangazawa na vyomvo vya habari, mkutano huo kati ya Serikali na  viongozi wa wafanyakazi haukufikia muafaka na wamekubaliana kukutana tena siku nyingine. Kitendo cha kukutana halafu wasifikie mfaka ni ishara kwamba hili ni sula zito sana na limewasumbua sana wafanyakazi na hivyo imekuwa vgumu kuridhishwa na ufafanuzi wa Serikali.

Kuna mengi ya kujifunza kutoka kwenye tukio hili. Kwanza, tumejifunza kwamba mshahara ndiyo chanzo kikubwa cha kipato  kinachotegemewa na wafanyakazi na huenda ni chanzo pekee kwa wafanyakazi wengi. Pili, mshahara ni mdogo na hautoshi kukidhi mahitaji ya wafanyakazi na ndiyo maana wamelalamika. Wangekuwa na vyanzo vingine vya kipato au mshahara ungekuwa unawatosha, kusingetokea malalamiko hayo yaliyotokea.

Malalamiko ya wafanyakazi kuhusu mshahara si kitu kitu kipya. Ni malalamiko ya miaka yote na yamekuwa yakisikika katika majukwa mbalimbali kama vile sherehe za wafanyakazi (Mei Mosi). Hakuna risala nayotolewa na Wafanyakazi siku ya Mei isiyolalamikia kiwango kidogo cha mishahara. Kwa upande mwingine, hakuna siku ambayo Serikali imeweza kuongeza mishahara kiasi kikubwa cha kulinga na kile wanachoomba wafanyakazi. Hiyo haijawahi kutokea na kwa uzoefu uliop haitatokea. Hivyo tunaweza kuhitimisha kuwa kila mtu anajua kuwa mishahara haiwatoshi wafanyakazi na haitatokea iwatoshe.

Rafiki yangu mpendwa, umewahi kujiuliza, kama mishahara haitoshi, kwa nini wafanyakazi hawatafuti vyanzo vingine vya kipato na kuachana na kutegemea mshahara pekee yake? Au kwa nini hawaachi kazi ili watafute vyanzo vingine vya kipato vinavyoweza kutosha mahitaji yao? Je, wale ambao hawajaajiriwa kwanini kila anayemaliza masomo anataka kuajiriwa wakati anajua kabisa walioko kazini wanalalamikia mishahara wanayopata?

Mbaya ziadi ni kwamba siku hizi ajira ni chache, na watu wanaomaliza masomo ni wengi na wanachelewa sana kupata ajira. Pamoja na kuchelewa kupata ajira, mtu yuko tayari kuhangaika kwa miaka  hata kumi akitafuta ajira ili aje apate mshahara ambao unalalamikiwa kuwa ni mdogo badala ya kumaliza masomo na kwenda moja kwa moja kwenye shughuli nyingine isiyo ya kuajiriwa laikini itakayompatia kipato cha kuridhisha. Unaweza kujiuliza kwa nini hali iko hivi?

Maswali haya na mengineyo  ni maswali magumu sana ambayo huenda si rahisi kupata majibu yake bila kuangalia nini chanzo cha hali hii. Katika makala haya nitakushirikisha kwa ufupi kwa nini watu wanapenda sana kuajiriwa licha ya changamoto nyingi zilizopo kwenye ajira ikiwemo nafasi zinyewe za ajira kuwa chache na mishahara kuwa mdogo.

Pengine, kabla sijaendelea, niweke wazi kwamba kuajiriwa si kitu kibaya na sina nia ya kuwashawishi watu wote wenye sifa za kuajiriwa wasiajiriwe. Kuajiriwa kuna faida zake kwa waajiriwa wenyewe na kwa jamii nzima maana watu walioko kwenye ajira ndiyo wanatupatia  huduma mbalimbali zilizo muhimu kwetu na jamii kwa ujumla.

Sababu kubwa inayowafanya watu waendelee kuajiriwa na walioko nje ya ajira watamani kuajiriwa ni dhana iliyopitwa na wakati kuhusu ajira. Kwa miaka mingi sana kumekuwa na mtazamo katika jamii kwamba ajira ndiyo chanzo cha uhakika cha maisha bora. Kutokana na mtazamo huu, kila mtu alipambana kwa kadri awezavyo kusoma kwa bidii ili afaulu vizuri kwa lengo la kuwa na kazi nzuri itakayompatia kipato cha uhakika maisha yake yote ya ajira na baada ya ajira atapata mafao ya kustaafu yatakayomwezesha kumalizia maisha yake yaliyobaki. Hata wazazi, walezi, walimu na jamii kwa ujumla wamekuwa wakiwambia watoto kwenda shule, wasome kwa bidii ili wafaulu na kupata kazi nzuri itakayowezesha kuishi maisha mazuri kabla na baada ya kustaafu.

Kutokana na dhana kwamba ajira ndiyo njia ya uhakika ya kuwa na maisha bora, waajiriwa wengi wanadhani kuwa hakuna maisha mazuri nje ya ajira na hivyo hawako tayari kufanya shughuli nyingine ya kujipatia kipato tofauti na ajira. Dhana hii imewafanya watu walioko kwenye ajira waendelee kuwa kwenye ajira na wale wasio kwenye ajira watafute kuingia kwenye ajira.

Vilevile, zipo sheria zinazojenga mazingira kwa waajiriwa kuendelea kuajiriwa. Kwa mfano, kwa mujibu wa sheria za hifadhi ya jamii, ili mwajiriwa apate mafao ya kustaafu, anatakiwa afanye kazi kwa jumla ya angalau miezi 180 (miaka 15) na hata kama ametimiza miaka hiyo haruhusiwi kuanza kupata mafao ya pensheni hadi afikishe umri wa kustaafu kwa mujibu wa sheria ambayo kwa sasa hapa Tanzania ni miaka 55 kwa hiari na 60 kwa lazima. Kama mtu ataacha kazi kabla ya kufanya kazi kwa miaka 15 hawezi kupata mafao ya pesheni. Sheria kama hizi zinawafanya watu watafakari mara mbili kabla ya kuamua kuacha ajira ili wafanye shughuli zingine zenye kipato kizuei zaidi.

Kwa upande wa vijana ambao bado hawajaajiriwa, nao wameshanasa kwenye mtego wa ajira. Vijana hawa wameshaaminishwa kwa muda mrefu na hata mfumo wa elimu umewaandaa kufikiri kuwa maisha ni ajira na hakuna maisha ya uhakika nje ya ajira.

Hata wale wachache wenye ndoto ya kujiajiri, kufanya biashara na uwekezaji nao huwa wanatamani kupata ajira kwanza ili kujihakikishia usalama wa maisha na baadaye ndiyo wafanye shughuli za ndoto zao. Kwa bahati mbaya, wakishaingia kwenye ajira, wengi huishia kuwa waajiriwa kwa maisha yao yote na wachache wanaofanikiwa kuachana na ajira, wengi wao hufanya hivyo wakiwa wamechelewa sana.

Unahitaji maarifa na nguvu ya ziada ili kujinasua kwenye mtego huu. Unahitaji kuangalia uhalisia ili uweze kujua kwamba lolote linawezekana, iwe ni kwenye ajira au nje ya ajira. Na unahitaji uweze kufanya maamuzi yako mwenyewe, kuyasimamia na kutokusikiliza wanaokukatisha tamaa. Hapo ndipo utaweza kuondoka kwenye mtego wa ajira.

Ili uweze kupata maarifa yatakayokufungua na kukufanya ufikirie nje ya boksi la kuajiriwa tu, unahitaji kupata elimu ya fedha ambayo haifundishwi darasani.Ukipata elimu hiyo utaweza kufikiria njia mbadala ya kujipatia kipato badala ya kufikiria ajira pekee.  Elimu hiyo utaipata kutoka kwenye vitabu vizuri kuhusu elimu ya msingi ya fedha. Mojawapo ya vitabu hivyo ni kitabu kiitwacho:

 SIRI ZA MAFANIKIO YA KIFEDHA KATIKA NDOA NA FAMILIA: Kanuni za Kibiblia na Kiuchumi na Kukabiliana na Migogoro na Changamoto za Kifedha Katika Ndoa na Familia.

Ili kupata maelezo zaidi kuhusu kuhusu kitabu hiki bonyeza hapa

.

About Simeon Shimbe

Simeon Shimbe ni mchumi kitaaluma, mwandishi wa vitabu na makala na mjasiriamali. Amekuwa akiandika kuhusu masuala ya fedha, biashara na uwekezaji na masuala mbalimbali ya kiroho.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *